1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrika katika magazeti ya Ujerumani

Abdu Said Mtullya30 Mei 2014

Wiki hii magazeti ya Ujerumani yanauzingatia ushindi wa Jenerali Abdel Fattah al-Sisi katika uchaguzi wa nchini Misri. Pia yameandika juu ya Boko Haram na biashara ya Uran baina ya Ufaransa na Niger

https://p.dw.com/p/1C9dp
Wafuasi wa Jenerali Abdel Fattah al Sisi nchini Misri
Wafuasi wa Jenerali Abdel Fattah al Sisi nchini MisriPicha: DW/Mostafa Hashem

Gazeti la "die tageszeitung" limeandika juu ya uchaguzi wa Rais nchini Misri. Jenerali Abdel Fattah al-Sisi alishinda katika uchaguzi huo kwa kupata karibu asilimia 97 ya kura.

Gazeti la "die tageszeitung" linasema Jenerali Abdel Fattah al-Sisi ameshinda uchaguzi wa nchini Misri kwa kishindo,kama ilivyotarajiwa.Mshindani wake wa pekee, mwanaharakati wa mrengo wa shoto Hamdin Sabahi aliambulia asilimia tatu. Walioshiriki katika kupiga kura walikuwa asilimia 48 .

Mwenyekiti wa ujumbe wa Umoja wa Ulaya ulioufuatilia uchaguzi huo Robert Goebbels amesema kuwa uchaguzi uliifuata misingi ya kidemokrasia na ulifanyika kwa amani lakini haukuwa wa haki katika ngazi zote.Gazeti la "die tageszeitung" limewanukuu Udugu wa kiislamu wakisema kuwa ni asimilia 11 .82 tu ya wastahiki waliopiga kura

Boko Haram

Gazeti la "Süddeutsche" limeandika juu ya mkasa wa kusikitisha wa mama mmoja maarufu wa Nigeria.Mama huyo anaeitwa Obiageli Ezekwesili mwenye watoto watatu wavulana, wakati wote alikuwa ndoto ya kumpata mtoto wa kike.Baada ya muda alijaaliwa kumpata msichana. Lakini msichana huyo ni miongoni mwa watoto zaidi ya 200 waliotekwa nyara na magaidi wa Boko Haram.

Gazeti la "Süddeutsche" limearifu kwamba mama huyo maarufu sana nchini Nigeria sasa anawaongoza wanaharakati wanaokutana kila siku katika mji mkuu wa Nigeria, Abuja kuendesha kampeni ya kuishinikiza serikali ili ichukue hatua za kuwakomboa, na kuwarudisha nyumbani salama wasichana waliotekwa nyara.

Gazeti la "Neues Deutschland" wiki hii limechapisha makala ya Wolf Christian Paes juu ya vita vya kupigania mamlaka katika Sudan Kusini.Jee vita hivyo vitakwisha? Katika makala yake Wolf Christian Paes alieitembelea Sudan Kusini anasema kuwa yapo matumaini.

Jee mgogoro wa Sudan Kusini utakwisha?

Paesanaeleza katika makala yake kwamba tokea kuanza kwa mapambano baina ya wapiganaji wa Rais Salva Kiir na waasi wanaomuunga mkono aliekuwa Makamu wa Rais, Riek Machar makubaliano kadhaa ya kusimamisha mapambano yametiwa saini. Lakini karibu yote yamekiukwa.Jee wapiganaji hawazifuati amri za makamanda wao?

Christian Paes anasema katika makala yake kwamba makubaliano ya kusimamisha mapigano yaliyotiwa saini tarehe 9 mwezi wa Mei baina ya Rais Salva Kirr na Riek Machar mjini Addis Ababa ni hatua inayoeleka kwenye lengo sahihi. Amesema inapasa kutambua kwamba hapo awali wanasiasa hao walikataa kabisa hata kukutana. Lakini sasa Rais Kiir na Riek Machar wamekubaliana kusimamisha mapigano. Hiyo ni hatua inayoelekea kwenye mchakato wa amani katika Sudan Kusini.

Hata hivyo Wolf Christian Paes amesema alichoweza kukishuhudia katika nchi hiyo ni kwamba mapambano ya kupigania mamlaka hayawezi kutenganishwa na vita vya kikabila ingawa wasomi wa nchi hiyo wanajaribu kukanusha.

Biashara ya madini ya uran

Gazeti la "die tageszeitung" wiki hii limeandika juu ya biashara ya madini ya Uran baina ya kampuni ya Ufaransa Areva na serikali ya Niger.

Gazeti hilo linaeleza kwamba mkataba juu ya kuyazalisha madini hayo umetiwa saini baina ya kampuni hiyo ya Ufaransa na serikali ya Niger. Kwa mujibu wa wachunguzi mkataba huo ni hatua ya kuumaliza unyonyaji uliokuwa unafanywa na makampuni ya nje nchini Niger.Serikli ya nchi hiyo imefurahishwa na mkataba huo.Hata hivyo gazeti la die "tageszeitung" linauliza jee wananchi wa Niger watanufaika na mktaba huo.?

Gazzeti hilo limeunukuu utafiti wa shirika la misaada la Oxfam .Kwa mujibu wa utafiti huo uzalishaji wa madini ya Uran nchini Niger baina ya kampuni za Ufaransa na za Niger mnamo mwaka wa 2010 uliingiza Euro Bilioni 3,5. Lakini Niger ilipata Euro Milioni 459 tu.

Mwandishi:Mtullya Abdu/deutsche Zeitungen.

Mhariri:Yusuf Saumu